Na Naamala
Samson
Waziri Mkuu wa serikali ya awamu ya
nne, Mhe. Mizengo Pinda, amewahimiza vijana wa kitanzania kujishughulisha na
kilimo na ufugaji wa kisasa ili kupata matokeo bora na kuinua kipato chao na
cha taifa kwa ujumla.
Mhe.Pinda aliyasema hayo mwishoni mwa wiki shambani kwake katika kijiji cha Zuzu mkoani Dodoma alipotembelewa na umoja wa wajasiriamali vijana wa GO BIG MOVEMENT wapatao arobaini na mbili (42) waliokuwa katika ziara ya kujifunza kwa vitendo kuhusu ukulima na ufugaji wa kisasa.
Aliwahimiza vijana hao kutokata
tamaa pindi wanapopata changamoto mbalimbali katika kufanikisha ndoto zao za
kumiliki ardhi kubwa nchini na kuitumia kujiajiri na kuwaajiri wengine kupitia
kilimo.
Akizungumza na vijana hao
aliwaambia, “Makundi mengi yameshanitembelea hapa na kueleza changamoto zao
lakini GO BIG MOVEMENT mmekuja kitofauti sana na kwa siku nyingi tangu nikiwa
waziri mkuu nilikuwa natafuta vijana wa mfano kama ninyi”.
Aliongezea kwa kusema, “Mna fursa
nyingi sana za kufanya kilimo cha kisasa na hata ufugaji wa kisasa zaidi yangu
kwani maarifa yapo nje nje na pia mtaweza kusaidiwa na serikali pamoja na
taasisi mbalimbali za kifedha kupitia umoja wenu huu”.
Katika ziara hiyo iliyochukua
takribani masaa nane, vijana hao wakiongozwa na kiongozi wao Bw.Meshack Maganga,
walipata nafasi ya kumuuliza maswali mbalimbali Mhe.Pinda na kisha kuzunguka
katika shamba la ekari hamsini (50) lenye mazao mbalimbali kama vile mapapai,
miembe, zabibu, migomba, maparachichi na viazi. Pamoja na kuona kilimo,
waliweza pia kuona ufugaji wa nyuki, bata, kuku, ng’ombe, mbuzi , kondoo na
hata uzalishaji wa nishati ya umeme kwa kutumia upepo na kinyesi cha ng’ombe
“biogas”.
Aidha, waziri mkuu mstaafu alizidi
kusisitiza vijana wa kitanzania kujiunga katika vikundi vya kijasiriamali ili
waweza kujikwamua kiuchumi. Vilevile katika ziara hiyo, Mhe.Pinda aliweza
kuwakutanisha vijana hao na mkurugenzi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC)
Bw.Nehemia Mchechu ambaye nae hakusita kuwapongeza kwa kuthubutu kuanza safari
ya kuwekeza kwenye ardhi hasahasa kufanya kilimo na ufugaji wa kisasa.
“Kiukweli ninaliona taifa la
Tanzania likiwa linainuka na kufanikiwa kufuta umaskini kupitia kwenu. Na nitajitahidi
kuwasaidia kadri niwezavyo ili muweze kutimiza ndoto zenu ikiwa hasahasa ya
kumiliki ardhi na nyumba za bei nafuu kama ilivyo nia ya Shirika la Nyumba la
Taifa” Aliongezea Bw.Mchechu.
Baada ya kuzunguka shamba hilo,
Mhe.Pinda aliwasisitiza vijana hao kuwa wajasiriamali wabunifu na wenye maono
ya kuzalisha vitu vyenye ubora ili viweze kukidhi masoko ya ndani na ya
kimataifa kwani tatizo lililopo ni wazalishaji kutofikia viwango vinavyotakiwa
na walaji.
Kwa upande wake Bw.Maganga
alimshukuru waziri mstaafu huyo kwa kuwapokea kwa heshima kubwa na kuahidi
kuendelea kujifunza daima kupitia wakulima, wafugaji na wajasiriamali wengine
wakubwa. “Mheshimiwa waziri mkuu mstaafu tukuhakikishie tu haya tuliyojifunza
kwako hatutayaacha yapotee, bali tutayafanyia kazi ili kuhakikisha tunajiinua
kiuchumi na kuendeleza taifa letu.”
Bw.Maganga akielezea historia
fupi ya GO BIG MOVEMENT mbele ya Mhe.Pinda (Picha na Naamala Samson)
Bw.Nehemia Mchechu akisisitiza
jambo (Picha na Naamala Samson)
Mhe.Pinda akiwatembeza vijana wa
Go Big shambani kwake (Picha na Naamala Samson)
Baadhi ya mifugo iliyopo shambani
kwa Mhe.Pinda (Picha na Naamala
Samson)
Mhe.Pinda akikabidhiwa fulana na
viongozi wa Go Big, kushoto ni Malaika na Bw.Maganga akiwa katikati (Picha na
Naamala Samson)
Vijana kutoka umoja wa
wajasiriamali wa GO BIG MOVEMENT wakiwa katika picha ya pamoja na Mhe.Pinda