Chama
cha Wamiliki/Waendeshaji wa Mitandao ya Kijamii nchini 'Tanzania
Bloggers Network' (TBN) kinasikitishwa na kulaani vitendo vya baadhi ya
Vyombo vya Habari kutumia kazi za wanachama wake (picha, video, habari)
bila idhini na bila kutoa maelezo stahiki ya vyanzo vya kazi hizo.
Taarifa iliyotolewa na Kamati ya Uongozi TBN Taifa Julai 11 mwaka huu, inaeleza masikitiko yake hayo kufuatia
Gazeti la kila siku la Majira, toleo namba 8217 la Alhamisi Julai 7,
2016 ambalo bila aibu lilichukua picha katika Mtandao wa Michuzi Blog
ina kuitumia pamoja na malezo yake bila ridhaa wala kutoa kueleza
chanzo cha hiyo picha.
Juu ni picha inayolalamikiwa kuwa imetumiwa na gazeti la majira na chini ni picha hiyohiyo ikiwa na logo ya Michuzi blog ambaye ndiye aliyehusika kuipiga
Katika picha ambayo ilitumiwa na gazeti hilo, Wahariri wa Majira kwa makusudi waliondoa alama maalum ya kumbukumbu iliyowekwa katika picha hiyo (watermark-logo) na kuichapisha katika ukurasa wa mbele wa gazeti hilo, bila kutaja chanzo chake, jambo ambalo ni ukiukwaji wa Sheria na kinyume na taaluma ya habari.
"Kitendo
hicho ambacho pia kimekuwa kikifanywa na baadhi ya magazeti hapa nchini
kimeonesha dhahiri ni jinsi gani baadhi ya vyombo vyenye tabia hiyo
visivyothamini kazi za ‘bloggers’ na mchango wake kwenye tasnia nzima,
huku wakiendelea kulea waandishi na wapiga picha wavivu na wazembe
wanaotumia blogs kama njia ya mkato kupata material" inaeleza taarifa hiyo
Hata hivyo TBN kwa kutambua kuwa si vibaya vyombo vya habari kutegemeana ama
kushirikiana kwa kutumia kazi za chombo kingine lakini inasisistiza kuwa
ni vema chombo kinachotumia kazi ya mtu mwingine kumtambua kwa kumtaja
katika kazi hiyo ama kukubaliana na chombo husika kabla ya kufanya
hivyo.
"Chama
cha Wamiliki/Waendeshaji wa Mitandao ya Kijamii nchini hakitafumba
macho kuona kazi za wanachama wake zikitumiwa na vyombo vingine vya
habari bila utaratibu na wala makubaliano ya kabla kwa wahusika" Inaeleza zaidi taarifa hiyo